Tuesday, October 15, 2013

DALALI WA NYUMBA AMBAKA MTOTO WA MIAKA SITA NA KUMJERUHI VIBAYA.....




Dalali wa viwanja na nyumba eneo la Mbezi Makabe, jijini Dar es Salaam anatuhumiwa kumbaka mtoto wa miaka sita na kumjeruhi vibaya sehemu zake za siri.
Tukio hilo limetokea Septemba 3, mwaka huu, ambapo mtoto huyo (jina linahifadhiwa) alifanyiwa unyama huo na dalali huyo anayejulikana kwa jina moja la Mgosi.
Akizungumza kwa masikitiko na gazeti hili, mama mkubwa wa mtoto huyo, Elizabeth Aloyce (28), alisema Mgosi ambaye ni dalali wa viwanja na nyumba katika eneo hilo, alikuwa akimfanyia kitendo hicho kwa muda mrefu.
Alisema kugundulika kwa tabia hiyo chafu ilikuja baada ya mtoto huyo kushindwa kutembea kutokana na maumivu makali.
Elizabeth alidai kwamba siku ya tukio alirudi nyumbani mapema kutoka kwenye biashara zake, alipoingia ndani alimkuta mtoto huyo amelala huku akiugulia.
Alipomuuliza kitu gani anachoumwa, mtoto huyo alianza kulia huku akificha sehemu zake za siri.
"Nilishtuka sana kuona hali ile, nilimshika na kuanza kumchunguza ndipo nikagundua sehemu zake za siri zimeharibika na kibaya zaidi mbegu za kiume zilikuwa zimeenea kila mahali," aliongeza kusema.
Kutokana na hali hiyo, aliamua kuwaita majirani na baada ya kushuhudia walikiri mtoto huyo amebakwa.
Baada ya kugundua suala hilo walimbana mtoto huyo amtaje mtu aliyemfanyia kitendo hicho, ndipo alipomtaja jina la mtuhumiwa na kwamba ilikuwa siyo mara yake ya kwanza kufanyiwa kitendo hicho.

MTOTO ANENA
Mtoto huyo akiongea na NIPASHE alisema kabla ya kufanyiwa unyama huo, mtuhumiwa huyo alikwenda kumchukua wakati akicheza na watoto wenzake.
"Nilikuwa nacheza alikuja Mgosi na kunichukua hadi chumbani kwake na kunilalia juu, kila siku ananifanyia hivyo na kuniambia nisiseme kwa mtu atanipiga," alisema mtoto huyo.
Alisema siku ya mwisho mtuhumiwa huyo mara baada ya kumaliza haja zake alimwambia arudi nyumbani kwao haraka.
"Nilirudi nyumbani niliogopa mama atanikuta nikitoka kwa mgosi, lakini niliona maumivu makali," aliongeza kusema.

POLISI WAMKAMATA
MTUHUMIWA
Baba mzazi wa mtoto huyo (jina linahifadhiwa) alisema tukio waliliripoti kituo cha Polisi Mbezi kwa Yusufu baada ya kumaliza taratibu zote za kumpatia matibabu Hospitali ya Rufaa ya Tumbi.
Polisi walifanikiwa kumkamata mtuhumiwa huyo na kukaa ndani kwa siku kumi, kisha kuachiwa kwa dhamana.
Hata hivyo, alisema hajaridhishwa na mwenendo wa suala hilo baada ya polisi wa kituo hicho kumzungusha kwa muda mrefu na hakuna dalili ya kumfikisha mtuhumiwa mahakamani.
"Tumekatishwa tamaa na utendaji wa polisi, hivi sasa imefikia muda wa mwezi mmoja hakuna kilichofanyika huku mtuhumiwa ameachiwa huru," alisema.
POLISI YATOA TAMKO
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ilala, Camilius Wambura, alipoulizwa kuhusu tukio hilo, alisema halifahamu na kuahidi kulifuatilia kwa kina ili aweze kutolea ufafanuzi.
Hata hivyo, aliwataka wananchi kutambua wajibu wa jeshi hilo siyo tu kumfikisha mahakamani mtuhumiwa, badala yake inawajibika kufanya upelelezi kisha jalada husika kulipeleka kwa mwanasheria wa serikali kwa ajili ya kuchukuliwa hatua.
"Naomba wananchi wafahamu kwamba polisi kazi yao ni kupeleleza tu, kazi ya kufikisha mahakamani ni Ofisi ya mwendesha mashtaka wa serikali (DPP), hivyo kutupa lawama ni kutuonea," alisema Kamanda Wambura.
Alisema hata suala la mtu kupewa dhamana lipo kisheria na kila mtu ana haki ya kudhaminiwa, bali kwa makosa machache ya jinai kama kuua, wizi wa matumizi ya nguvu, biashara ya madawa ya kulevya ndiyo mtuhumiwa wake hawezi kupewa dhamana.
CHANZO: NIPASHE JUMAPILI  
    source boss ngasa 

No comments:

Post a Comment